Tuesday, May 29, 2012

MSHAURI WA CHADEMA MBEYA AMTUPIA KOMBORA MWENYEKITI WAKE


MSHAURI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA)Mkoa wa Mbeya,Bw. Eddo Mwamalala  amemtupia kombora Mwenyekiti wa Chama hicho Wilaya ya Mbeya mjini Bw.John Mwambigija kuwa siasa zake majukwaani  ni za uchochezi ambao haupaswi kufumbiwa macho.

Aliyasema hayo juzi katika mkutano na waandishi wa habari uliofanyika kwenye Hoteli ya Mbeya Peack mjini hapa huku lawama hizo pia akilitupia Jeshi la Polisi mkoani hapa kwa maelezo kuwa Polisi wamekuwa wakimfumbia macho Bw.Mwambigija.

Bw.Mwamalala ambaye pia ni mjumbe wa mkutano mkuu wa Taifa alisema kuwa,Bw.Mwambigija amekuwa akiyatumia majukwaa kwa kutoa lugha za matusi na vichekesho kitendo ambacho kinaweza kuhatarisha amani ya watanzania.

Katika mkutano huo Bw.Mwamalala aliwaambia waandishi kwamba ,anashangazwa pia na ukimya wa katibu mkuu wa Chadema Bw.Wilbrod Slaa kuendelea kukaa kimya bila ya kukemea tabia hiyo ya Mwenyekiti huyo.

“ Nalishangaa sana jeshi la polisi kwa kuendelea kumwangalia huyu mtu kauli anazotoa akiwa jukwaani ni za uchochezi kwani lugha nyingi ni za matusi lakini polisi wamekuwa wakimwangalia hata katibu mkuu Dr.Slaa amekaa kimya bila ya kukemea vitendo hivyo.’’Alisema

Aidha,aliongeza kuwa kutokana na lugha za matusi na vichekesho visivyo na tija katika jamii amekuwa  akishangiliwa na wananchi na kupata kiburi akijigamba na kusema yeye ndiye aliye mpa madaraka Mbuge Joseph Mbilinyi na madiwani kupitia tiketi ya Chadema mkoani hapa.

Mshauri huyo aliendelea kuponda  akisema kwamba Bw.Mwambigija ni tatizo ndani ya Chadema maana kazi yake ni kuchekesha watu majukwaani, kutukana na kuendelea kutoa matamko yasiyo na tija kwa wanachama huku akiwarubuni baadhi wa wanawake akiomba magari yao kwa ajili ya misafara isiyo rasmi kwa ushawishi wa  kuwateua kwenye ubunge wa viti maalumu.

.
Bw.Mwamalala alisema kuwa Viongozi wa Chadema kuendelea kulifumbia macho suala la Mwambigija ni kukibomoa chama badala ya kukijenga.

Alisema kutokana na mambo hayo tayari Bw.Mwambigija ambaye ni maarufu kwa jina la Mzee wa upako mnamo Juni 4 mwaka huu atapandishwa kizimbani kusomewa shitaka kwa mara ya kwanza.

Bw.Mwambigija katika mahojiano mafupi na majira kwa njia ya simu alikiri kwamba siku hiyo atasomewa shitaka baada ya kushitakiwa na aliyekuwa Mwenyekiti wa Chadema Wilaya ya Chunya Bw.George Ntasha Katabi akituhumiwa kumtolea lugha za kashfa katika moja ya mkutano.

No comments:

Post a Comment