Monday, May 21, 2012

WAANDISHI WA HABARI WAPEWE FURSA KWENYE ZIARA ZA VIONGOZI MIKOANI

KATIKA   ziara za viongozi wa kitaifa mikoani,  zinaonekana kuwa na mapungufu ya kuikosesha jamii kile kinacho kusudiwa kuwafikia.

Nalazimika kuyasema haya kufuatia dosari zilizojitokeza hivi karibuni katika ufunguzi wa mbio za Mwenge Mkoani Mbeya.

Mheshimiwa Waziri mkuu Mizengo Pinda ndiye aliyefungua mbio hizo, lakini awali ya yote siku moja kabla ya kuanza kwa mbio hizo mnamo Mei 10 kwenye Ikulu ndogo ya mkoa wa Mbeya, kulitokea mkanganyiko ambao unaweza kuwa chanzo cha kuinyima jamii haki yao ya msingi ya kupata habari.

Wanahabari ni muhimili wa nne katika  serikali yetu ikitanguliwa na serikali kuu,sheria na Bunge.

Wajibu wao mkubwa ni kuhakikisha kwamba wanaifikishia jamii taarifa ya serikali kwa mujibu wa kanuni na maadili ya tasnia yao. Lakini kile kilicho jitokeza siku hiyo ni sehemu ya mapungufu ambayo hayastahili kurudiwa.

Naamini kwamba, bajeti ya mkoa katika shughuli zote kuhusiana na mbio za mwenge ilizingatia umuhimu na heshima ya mbio hizo ambazo imekuwa ni sehemu ya utamaduni wa watanzania tangu enzi  za uhai wa mwasisi wa mbio hizo, Baba wa Taifa Mwl. Julius Kambarage Nyerere.

Katika bajeti hiyo waandishi hawakupewa umuhimu wa juu kama muhimili wa nne katika Taifa kwa kushindwa kuwaandalia usafiri wa kutosha ili kufika katika maeneo mbali mbali aliyopangiwa kiongozi wa serikali,Mh.Pinda

Naamini kwamba si wananchi wote ambao walikuwa na fursa ya kufika alikotembelea  Waziri mkuu,kwa maana hiyo msaada wao mkubwa ulikuwa ni kupata taarifa kwa upana kupitia vyombo vya habari.

Lakini kwa sababu idadi kubwa ya waandishi wa habari walishindwa kuambatana na msafara wa Waziri mkuu, kutokana na kukosa usafiri, naamini hata katika upashaji wa habari kwa jamii haukukidhi mahitaji ya wananchi hasa ukizingatia kwamba tukio hilo la mbio za mwenge lilikuwa tukio kubwa la kitaifa mkoani humo.

Nadhani jambo la kwanza la kuzingatia lilikuwa ni kuhakikisha wananchi wanapata ujmbe wa mbio hizo na agizo la kiongozi wao kupitia vyombo vya habari ,hivyo basi waandishi walitakiwa kuandaliwa mapema mazingira ya kuweza kufanya kazi zao kwa maslahi ya jamii.

Najua zipo sababu ambazo zinaweza kutolewa za kushindwa kuwaandalia waandishi usafiri wa kuongozana na msafara wa Mh.Pinda kabla ya kuzindua mbio hizo za mwenge alipo kuwa akienda kukagua Kiwanda cha Tanganyika Packers,kiwanda cha Marumaru na kituo cha utafiti wa kilimo Uyole.

Lakini sababu hizo nadiliki kusema kuwa zinaweza kuwa hazitalingana na umuhimu wa wanahabari katika kuitumikia jamii,moja kwa moja, nadhani sababu ambazo zinaweza kutajwa  labda inaweza kuwa ni ufinyu wa bajeti kuhusu ugeni huo kwa maana kuwa waandaji walihofu namna ya kuwawezesha (posho) waandishi.

Afisa habari wa ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Mbeya anapaswa kujua mahitaji ya wananchi kupitia waandishi wa habari,hili ndilo jambo la msingi. Posho ni jambo la ziada japo si kweli kwamba ofisi ingeshindwa kufanya hivyo ,kwa sababu hawakupewa umuhimu ndio sababu zilizo sababisha kuwepo usumbufu wa usafiri.

Katika hili pia ni vema nikiwa wazi kwamba si waandishi wote ambao wanategemea kupewa posho ili waweze kumudu kazi zao,hapana.Nia ya mwandishi ni kupata habari na kuitangazia jamii kile ambacho kinaonekana kuwa na umuhimu.

Na kwa kuwa waandishi ni kama daraja la kuwaunganisha  viongozi  na wananchi ,waandishi wanaitumia fursa kama hiyo ili kuzitumikia pande zote mbili bila kujali posho.Jambo la msingi wasinyanyapaliwe kwenye vyombo vya usafiri kama ilivyo tokea katika gari moja aina ya Land cruiser lenye namba za usajili DFP 5950.

Dereva wa gari hilo na afisa habari wa ofisi ya mkuu wa mkoa kwa pamoja walitoa lugha ambazo ziliwafedhehesha waandishi wakati  wakitaka waandishi wapungue ndani ya gari hilo,si mara ya kwanza waandishi kufanyiwa vituko na watu hao.

Kwa lugha za nyodo afisa habari huyo bila kuzingatia taaluma ya wanahabari aliwataka waandishi wajitegemee usafiri kwa madai kuwa gari lililokuwa limeandaliwa kwa ajili yao lilikuwa na uwezo wa kubeba waandishi kumi tu,ndani ya gari hilo kulikuwa waandishi 11 lakini kutokana na kauli hizo baadhi ya waandishi waliamua kutelemka na kutawanyika .

Hali hiyo imesababisha idadi kubwa ya waandishi kususia mbio za mwenge huku kukiwa na malalamiko kwamba afisa habari amekuwa akiwatumia marafiki zake wanahabari katika ziara za viongozi mkoani hapa na kitendo hicho kimekuwa kikijirudia mara kwa mara.

Afisa habari kama kweli ni mwanataaluma wa habari, anapaswa kubadilika ili kazi za viongozi zitangazwe kwa mapana na viongozi pia katika ziara zao wajulishwe kwa mapana kero za wananchi kupitia tasnia ya habari ndani ya ziara zao.


No comments:

Post a Comment