Tuesday, July 10, 2012

MACHIFU MBEYA KUHESHIMU MIPAKA YA UTAWALA WAO



MUUNGANO wa Jamii Tanzania (MJATA) hivi karibuni umewataka machifu mkoani hapa kuheshimu taratibu na mipaka ya utawala wao ili kujenga imani kwa jamii inayo wazunguka.

Hayo yalisemwa katika mkutano wa Machifu chini ya MJATA uliofanyika Julai 5 mwaka huu huko Igawilo jijini Mbeya.

Chifu aliye jitambulisha kwenye mkutano huo kwa jina la Julius Lyoto,alisema kuwa ili kujenga mahusiano mema na jamii machifu wanatakiwa kubadilika na kujenga misingi ya ushirikiano , kuheshimu taratibu na mipaka ya utawala.

Lyoto alitolea mfano wa machifu wa zamani akiwemo marehemu Chifu Adam Sapi kwamba walikuwa na utamaduni wa kutembeleana na kujadili maadili ya utamaduni,mila na desturi ili kuijenga jamii katika misingi hiyo.

Katika mkutano huo, mwenyekiti wa maadili ya Muungano wa Jamii Tanzania ambaye pia alijitambulisha kuwa ni katibu wa machifu Wilaya ya Mbarali,Ibrahim Mwalalila alisema kuwa kusudi la mkutano huo ni kujua kero za wanachama wa MJATA.

Alisema kwamba,muungano huo umekuwa ukipoteza wanachama wake kwa idadi kubwa na kuwepo mahudhurio finyu kwenye mikutano kinyume na mahudhurio ya awali hali ambayo imesababisha viulizo kwa viongozi.

Chifu Rocket Mwanshinga alipata fursa ya kuzungumza na kubainisha kero zinazo changia wanachama hao kujiondoa kwenye muungano huo kuwa ni uongozi mbaya uliopo madarakani,kutohusishwa kwenye maamuzi ya chama hali inayowafanya wajione wanaburuzwa.

Kero zingine alizo zitaja ni kutotekeleza ahadi za pesa ili kuendesha shughuli za utunzaji wa mazingira na kuhifadhi misitu majukumu ambayo ni miongoni mwa wajibu wa machifu hao.

Chifu Mwanshinga alisema kwamba , machifu pia wamekuwa wakidhalilishwa na uongozi uliopo madarakani kwa kitendo cha kupita maofisini kuomba misaada kwa visingizio kuwa ni agizo la machifu kitendo ambacho si cha kweli.

‘Machifu sio omba omba,wala hatuna tabia hiyo lakini tunashangazwa na tabia hiyo,mbaya zaidi hatusomewi hata hayo mapato badala yake tunmasomewa matumizi huku tukiendelea kuchangishwa pesa’.Alisema

Baada ya mkutano huo mwandishi wa habari hizi hakufanikiwa kumpata mwenyekiti wa MJATA ,Shayo Masoko Soja ambaye alitajwa kwenye mkutano kuwa anawaburuza machifu hao kwenye uongozi wake.

Muungano huo ulianzishwa na kusajiliwa mwaka 2009 ambao ulianzishwa kwa kusudi la kupambana na kuzuia maovu katika jamii yakiwemo ya upagaji wa nondo,mauaji ya maalbino na mengine mengi.


No comments:

Post a Comment