Friday, July 20, 2012

RAIS KIKWETE KUWASILI KESHO MKOANI MBEYA KWA ZIARA YA SIKU MOJA



KWA mara ya kwanza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Jakaya Kikwete anatarajia kutua kesho katika uwanja mpya wa ndege  wa Kimataifa wa Songwe uliopo wilaya ya Mbeya vijijini mkoani Mbeya kwa ajili ziara yake ya siku moja mkoani hapa.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake leo, Mkuu wa mkoa wa Mbeya Abbas Kandoro amesema kuwa Rais Kikwete atatua katika uwanja huo majira ya saa kumi za jioni na kuwaomba wananchi wa eneo hilo kujitokeza kwa ajili ya kumpokea.

Kandoro amesema kuwa katika maandalizi ya ujio wa Rais Kikwete mkoani Mbeya, kuna ndege ambayo ingefika leo katika uwanja huo kisha kesho Rais kutua na kupokelewa na viongozi wa mkoa wa Mbeya pamoja na wananchi.

Amesema Rais Kikwete akiwa mkoani Mbeya atapokea taarifa ya mkoa kisha atapumzika na kesho kutwa (Jumapili) ataelekea katika eneo la uzinduzi wa mradi mkubwa wa Majisafi na taka uliojengwa eneo la Swaya Jijini Mbeya ambako atapata taarifa za mradi huo akiwa na viongozi wa Serikali za Ujerumani na Jumuiya ya Ulaya.

Baada ya hapo Rais Kikwete kutembelea mtambo wa kusafisha Majisafi na kutibu maji na kupata maelezo kisha kuzindua mradi huo na kutoa nasaha zake, msafara wake utaondoka na kurejea ikulu ndogo kisha ataelekea uwanja wa ndege Songwe kwa ajili ya kuondoka mkoani Mbeya.

Kwa upande wake Mkurugenzi msaidizi Wizara ya Maji Mhandisi Mary Mbowe, amesema kuwa mradi utakaozinduliwa na Rais Kikwete ni kati ya miradi mitatu mikubwa iliyokuwa ikitekelezwa katika miji mitatu Tanzania.

Amesema Mradi huo ni kati ya miradi mitatu mikubwa inayojulikana kwa jina la Regional Centers Program ambayo imetekelezwa katika Jiji la Mwanza, mkoa wa Iringa na sasa Jijini Mbeya na kugharimu Kiasi cha Shilingi Bilioni 80.
 
Mradi huo ulianza katikati ya mwaka 2009 na msimamizi mkuu alikuwa Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji safi na taka Jiji la Mbeya na katika uzinduzi utakaofanywa wageni mbalimbali watahudhuria.

Mbowe amewataja wageni hao kuwa ni pamoja na Kamishina wa Maendeleo ya nchi za Ulaya, Balozi wa Ujerumani, viongozi wa Wizara ya Maji, wawakilishi wa Wizara ya fedha na wawakilishi wa baadhi ya Mamlaka za Maji katika Miji Tanzania.

Uwanja wa ndege wa Songwe atakaotua Rais Jakaya Kikwete umekamilika katika sehemu ya kutua na kurukia ndege lakini umekwama katika ujenzi wa jengo la Abiria kutokana na Serikali kudaiwa zaisi ya Sh. Bilioni 5 na Mkandarasi aliyejenga uwanja huo kampuni ya Kundan Singh Construction Ltd ya nchini Kenya.

Mbali na kukwama kwa ujenzi wa Jengo hilo la abiria, pia hakuna jengo la kurushia ndege na sababu imetajwa kuwa Serikali imekwama kumlipa mkandarasi wa jengo hilo kampuni ya Beijing Construction Ltd, ambapo imeelezwa kuwa kutokana na Serikali kuchelewesha malipo hayo inaweza kuburuzwa mahakamani kwa kukiuka mikataba waliyoingia na wakandarasi hao.

No comments:

Post a Comment