Wednesday, July 4, 2012

WANANCHI MBEYA WAITIKISA SERIKALI

Na Steve Jonas

WANANCHI wa kata ya Isongole katika Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe mkoani Mbeya wiki iliyopita waliweka vizuizi kwenye barabara ya kutoka Uyole kwenda Tukuyu ili kuishinikiza serikali itatue kero zao .

Vizuizi hivyo vilivyokuwa vimetawala katika barabara hiyo ni pamoja na uchomaji wa magurudumu kati kati ya barabara,mawe , magogo na makundi ya watu wa rika mbalimbali hali  iliyosababisha kukwama kwa huduma za usafiri na huduma nyingine za kijamii.

Kwa mujibu wa baadhi ya wananchi waliohojiwa na mwandishi wa habari hizi kwa nyakati tofauti, kwenye maeneo ya tukio hilo,wananchi walichukua uamuzi huo baada ya kuchoshwa na vitendo vya kifisadi vinavyofanywa kwenye kizuizi cha kutoza ushuru wa mazao kilichopo eneo la Kijiji cha Namba Wani.

Daud Gabriel mkazi wa kijiji cha Ndaga alisema kuwa hatua ya wananchi kuzuia barabara hiyo ilitokana na kero za muda mrefu ambazo zimekuwa zikifanywa na watoza ushuru wa mazao ambao inadaiwa kwamba kuna ubaguzi unafanywa katika zoezi hilo.

Alisema kuwa kusudi la wananchi ni kutaka uwiano wa ushuru katika mazao yote kinyume na hivi sasa ambapo viazi hutozwa kiasi cha shilingi 120,000 kwa tani tano wakati ndizi na miwa hutozwa kiasi cha shilingi 30,000 kwa tani tano.

Naye Herman Ulaya alisema kwamba watoza ushuru hao wanatumia ubabe kwa kuwanyanyasa wananchi na kuwadhalilisha huku akitolea mfano kwake kuwa aliwahi kukamatwa akiwa na mzigo wa kuni kwaajili ya matumizi ya nyumbani.

Alisema alipelekwa katika kituo cha Polisi cha Kiwira na baadae alitozwa shilingi 160,000 kwaajili ya usumbufu kwa watoza ushuru kitendo ambacho alikielezea kuwa hakikuwa cha halali.

Mwenyekiti wa kijiji cha Ndaga,Paulos Said Zambi alizitaja kero za msingi kwa wananchi kuwa ni wananchi wanataka kutozwa ushuru kwa gharama zinazofanana bila kujali ni aina gani ya bidhaa.

Kero zingine ni kuitaka Halmashauri kuvipatia vijiji kiasi cha mapato yanayokusanywa,kulihamisha geti kwenda mpakani eneo la Isyonje na kuondoa ushuru wa mbegu zinazo pelekwa mashambani.

Zambi alisema kuwa wananchi wa vijiji nane vya kata ya Isongole wamekuwa wakitaabika kwa kipindi kirefu ambapo viongozi wamekuwa wakifumbia macho kilio chao hata kufikia hatua hiyo ya kuandamana na kufunga barabara ili viongozi waweze kujua umuhimu wa kilio hicho.

Wananchi hao waliandamana mnamo Julai 2 mwaka huu majira ya asubuhi na kusababisha vyombo vya usafiri kushindwa kufanya safari hali iliyosababisha msongamano wa magari hadi majira ya saa 11 jioni.

Askari wa jeshi la Polisi kutoka katika kituo cha kati jijini hapa walifika saa 8:40 wakiwa na silaha za moto na kufyatua hewani risasi mbili ambazo hazikufanikiwa kuwatawanya wananchi ambao walikuwa wakisikika wakisema ‘tunataka haki’.

Dakika 30 baadae mkuu wa mkoa wa Mbeya ,Abbas Kandoro akiongozana na kamanda wa Polisi wa mkoa wa Mbeya ,walifika katika kijiji cha Ndaga ambako Kandoro aliweza kutoa tamko la kuwataka wananchi hao wasitoe ushuru hadi hapo Halmashauri ya Wilaya itakapo kaa na kufika mwafaka.

Baada ya kauli hiyo ya mkuu wa mkoa iliyotamkwa majira ya saa 11jioni ,wananchi waliamua kuondoa vizuizi barabarani bila kushurutishwa na hali ilikuwa shwari mbali ya zoezi hilo kuwa kero kwa wasafiri ambao walilazimika kukwama wakati zoezi hilo likiendelea.

No comments:

Post a Comment